Amani, umoja na mshikamano vimetajwa kuwa ndio nguzo na misingi muhimu ya mafanikio na maendeleo yaliyofikiwa Zanzibar ndani ya miaka mitano iliyopita.
Fuatana na taarifa ya mwandishi wa TriGen Media aliyepo Paje, Mkoa wa Kusini Unguja…
Siri ya maendeleo makubwa ya watu na vitu, ikiwemo miundombinu ya kisasa Unguja na Pemba ndani ya miaka mitano tu ya utawala wa Dk. Hussein Ali Mwinyi, imetajwa kuwa ni amani na umoja miongoni mwa Wazanzibari.
Hayo yamesemwa na Dk. Mwinyi, ambaye ni mgombea urais wa Zanzibar kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) wakati wa mkutano wa kampeni uliofanyika Alhamisi, Oktoba 16, 2025, Paje, Kusini Unguja.

Dk. Mwinyi amesema CCM itaendelea kusimamia na kulinda misingi hiyo iliyoiwezesha Zanzibar kufikia mafanikio iliyonayo sasa.
Amesema sera kuu ya CCM imejikita katika kudumisha misingi hiyo kwa maendeleo ya taifa.
Amesema katika miaka mitano iliyopita, Zanzibar imepiga hatua kubwa kimaendeleo kutokana na mazingira tulivu na maridhiano ya kisiasa yaliyopo.
“Mpaka sasa katika miaka mitano iliyopita tumekwenda vizuri, nchi yetu ina amani, ina umoja, mshikamano, na hata tuna maridhiano ya kisiasa. Hii imesababisha mambo mengi ya kimaendeleo kufanyika kwa sababu ya amani tuliyokuwa nayo,” amesema.

Dk. Mwinyi amewaomba Wazanzibari wote kuendelea kulinda na kudumisha amani iliyopo, akisisitiza kuwa maendeleo hayawezi kupatikana katika mazingira ya mifarakano na ubaguzi.
Mbali na kuzungumzia masuala ya amani na umoja, Dk. Mwinyi ameahidi kuendeleza miradi mikubwa ya maendeleo katika sekta ya miundombinu ya usafiri na usafirishaji, hasa Mkoa wa Kusini Unguja, ikiwemo ujenzi wa mradi mkubwa wa barabara ya njia nne kutoka Tunguu hadi Makunduchi, mradi ambao utaufungua mkoa kiuchumi na kiutalii.
Amesema Serikali yake pia itahakikisha ujenzi wa madaraja mawili makubwa katika maeneo ya Kusini Unguja, yatakayorahisisha usafiri na kuongeza fursa za biashara na uwekezaji.



                                    